Proverbs 4

Hekima Ni Bora Kupita Vitu Vyote


1 aSikilizeni wanangu, mafundisho ya baba yenu;
sikilizeni kwa makini na mpate ufahamu.

2 Ninawapa mafundisho ya maana,
kwa hiyo msiyaache mafundisho yangu.

3 bNilipokuwa mvulana mdogo katika nyumba ya baba yangu,
ningali mchanga na mtoto pekee kwa mama yangu,

4 cbaba alinifundisha akisema,
“Yashike maneno yangu yote kwa moyo wako wote;
yashike maagizo yangu na wewe utaishi.

5 dPata hekima, pata ufahamu;
usiyasahau maneno yangu wala usiyaache.

6 eUsimwache hekima naye atakuweka salama;
mpende, naye atakulinda.

7 fHekima ni bora kuliko vitu vyote; kwa hiyo jipe hekima.
Hata ikikugharimu vyote ulivyo navyo, pata ufahamu.

8 gMstahi, naye atakukweza;
mkumbatie, naye atakuheshimu.

9 hAtakuvika shada la neema kichwani mwako
na kukupa taji ya utukufu.”


10 iSikiliza mwanangu, kubali ninachokuambia,
nayo miaka ya maisha yako itakuwa mingi.

11 jNinakuongoza katika njia ya hekima
na kukuongoza katika mapito yaliyonyooka.

12 kUtembeapo, hatua zako hazitazuiliwa;
ukimbiapo, hutajikwaa.

13 lMkamate sana elimu, usimwache aende zake;
mshike, maana yeye ni uzima wako.

14 mUsiuweke mguu wako katika njia ya waovu
wala usitembee katika njia ya watu wabaya.

15 Epukana nayo, usisafiri katika njia hiyo;
achana nayo, na uelekee njia yako.

16 nKwa kuwa hawawezi kulala mpaka watende uovu;
wanashindwa hata kusinzia mpaka wamwangushe mtu.

17 oWanakula mkate wa uovu,
na kunywa mvinyo wa jeuri.


18 pNjia ya wenye haki ni kama nuru ya kwanza ya mapambazuko,
ambayo hung’aa zaidi na zaidi mpaka mchana mkamilifu.

19 qLakini njia ya waovu ni kama giza nene;
hawajui kinachowafanya wajikwae.


20 rMwanangu, yasikilize kwa makini yale ninayokuambia;
sikiliza kwa makini maneno yangu.

21 sUsiruhusu yaondoke machoni pako,
yahifadhi ndani ya moyo wako;

22 tkwa sababu ni uzima kwa wale wanaoyapata
na afya kwa mwili wote wa mwanadamu.

23 uZaidi ya yote, linda moyo wako, kuliko yote uyalindayo,
maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.

24 Epusha kinywa chako na ukaidi;
weka mazungumzo machafu mbali na midomo yako.

25 vMacho yako na yatazame mbele,
kaza macho yako moja kwa moja mbele yako.

26 wSawazisha mapito ya miguu yako
na njia zako zote ziwe zimethibitika.

27 xUsigeuke kulia wala kushoto;
epusha mguu wako na ubaya.
Copyright information for SwhKC